BOKO HARAMU YAKIMBIZA MAMIA YA WANAIGERIA
POTISKUM, NIGERIA
Mamia ya wakazi wa mji wa kaskazini mwa Nigeria wa Potiskum wameyakimbia makazi yao wakihofia usalama wa maisha yao kutokana na hofu ya kundi la Boko Haram kufanya tena mashambulio dhidi ya mji huo.
Serikali ya Nigeria imeimarisha usalama katika mji huo baada ya kundi la Boko Haram kufanya mashambulio katika eneo hilo la kaskazini, ambapo watu 30 wanaripotiwa kuuawa.
Hali hiyo imewafanya raia wengi kuukimbia mji huo. Vikosi vya usalama vya Nigeria vinaonekana vikipiga doria na kurandaranda katika mitaa na barabara za mji huo. Aidha baadhi ya raia wanafadhilisha kubakia ndani na hawatoki nje wakihofia usalama wao.
Juzi jeshi la Nigeria lilimkamata mwanachama wa ngazi za juu wa kundi la Boko Haram ndani ya nyumba ya mjumbe wa Baraza la Kitaifa la Senate katika mji wa Maiduguri kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Kundi la Boko Haram lilianza kuzishambulia taasisi za kiserikali, kama vile magereza, vituo vya polisi na shule katika eneo la kaskazini mashariki mwa Nigeria tokea mwaka 2009, na hadi sasa limeshaua zaidi ya watu 1,500
AFRIKA YAPEWA TAHADHARI NA UN
NEW YORK, MAREKANI
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya
kibinaadamu amezitaka nchi za Kiafrika kuongeza juhudi za kupambana na tatizo
la chakula na vile vile kusimama imara katika kukabiliana na majanga ya
kimaumbile.
Catherine Bragg amesema hayo mwishoni mwa safari yake katika eneo
la kusini mwa Afrika na kuonya kuwa, eneo la kusini mwa Afrika linakabiliwa na
tatizo sugu la chakula na kwamba, uzalishaji chakula katika eneo hilo
umedhoofika kutokana na majanga mtawalia ya kimaumbile.
Amesema, theluthi moja
ya wananchi wa Lesotho hawana uwezo wa kukidhi mahitaji yao ya chakula.
Naibu
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya kibinaadamu amebainisha
kwamba, nchini Zimbabwe raia milioni moja na laki sita wanakabiliwa na hatari
ya tatizo la chakula na kwamba, familia nyingi zimekuwa zikiuza mifugo yao ili
ziweze kukidhi mahitaji yao ya chakula.
Ofisi ya Uratibu wa masuala ya
Kibinaadamu ya Umoja wa Mataifa imetoa taarifa inayobainisha kwamba, suala la
tatizo la chakula lingali tatizo kubwa katika eneo la kusini mwa Afrika hususan
katika nchi za Lesotho, Malawi, Swaziland na Zimbabwe.
Related Posts :
UGANDA YALITAKA KUNDI LA M23 KUSITISHA MAPIGANO
KAMPALA, UGANDA
Serikali ya Uganda imelitaka kundi la M23 la Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo lisianzishe tena mapigano ambayo yamewalazimisha maelfu
ya wakimbizi wa Kikongo kuvuka mpaka na kuingia nchini Uganda.
Wito huo
umetolewa na Okello Oryem, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Uganda ikiwa ni siku
moja tu baada ya Harakati ya Waasi ya M23 kutishia kwamba, itaanzisha tena
mashambulio dhidi ya vikosi vya serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Okello Oryem amesema, Kampala inalitaka kundi hilo kuheshimu usitishaji mapigano.
Kundi la M23 lilisitisha mapigano Agosti mwaka huu baada ya kukutana na Rais
Yoweri Museveni mjini Kampala na kutakiwa kufanya mazungumzo na serikali ya
Kinshasa.
Hata hivyo Runninga Lugerero, mmoja wa viongozi waandamizi wa M23
alitishia mwishoni mwa juma akiwa huko Bunagana kwamba, kundi lao litaanzisha
tena vita kutokana na kuwa, Rais Joseph Kabila wa Kongo hayuko tayari kufanya
mazungumzo ya amani.






